Saturday, September 13, 2014

Chaka Khan: Sauti iliyoacha historia kwenye miondoko ya Funk


 Unapozungumzia muziki wa Funk, hutatenda haki kwa mashabiki ikiwa hutamtaja Chaka Khan ambaye ni miongoni mwa wasanii waliowahi kufanya vizuri kwenye miondoko hiyo.
Kutokana na umahiri katika muziki wake msanii huyo alijijengea umaarufu mkubwa katika miaka ya 1970.
Jina lake lilianza kuwika alipojiunga na Bendi ya Rufus, iliyokuwa na maskani yake mjini Chicago, Marekani.
Wengi tunamfahamu kama Chaka Khan au Malkia wa Funk, lakini jina lake halisi ni Yvette Marie Sevens.Nyota huyu alizaliwa Machi 23,1953.
Nyota huyu mzaliwa wa Chicago, alionyesha mapenzi yake katika muziki tangu akiwa mdogo, jambo lililomfanya kufikiria kuacha shule ili aingie kwenye fani hiyo iliyomfanya kuwa miongoni mwa watu maarufu duniani.
Babu yake aliyekuwa akipiga muziki wa Jazz, ndiye alichangia kwa kiasi kikubwa Khan kuingia kwenye muziki,akiwa na umri wa miaka 11 tayari alishaanza kuonyesha kuvutiwa zaidi na miondoko ya R&B na Blues.
Mwaka 1969, Khan aliacha shule na kuanza kutumbuiza kwenye vikundi vya mtaani akiwa sanjari na mpenzi wake Hassan Khan, ambaye baadaye walifunga ndoa.
Khan aliingia rasmi kwenye muziki mwanzoni mwa miaka ya 70 akiwa mwanzilishi wa Kundi la Muziki la Crystalettes, lililokuwa likiundwa na wasichana ndugu wa familia moja.
Hata hivyo, kundi hilo halikudumu sana kabla ya kuvunjika na Khan kuhamia kwenye Bendi ya Rufus iliyokuwa ikisifika wakati huo katika miondoko ya Funk.
Sauti nzito aliyokuwa nayo mwanamama huyu ilimpa fursa ya kuwa muimbaji kiongozi katika bendi hiyo katika kipindi kifupi alichojiunga nayo.
Huo ndiyo ukawa mwanzo wa Chaka Khan kuingia kwenye ramani ya muziki wa Funk, hasa baada ya kuonyesha uwezo wa hali ya juu katika kuitumia sauti yake tamu kuwachezesha mashabiki wa miondoko hiyo.
Kupitia nyimbo ‘Tell Me Something’, ’Feel Good’, ‘Sweet Thing’, ‘Do you Love what you feel’ na nyinginezo Chaka Khan alifanikiwa kuifanya Bendi ya Rufus kujizolea umaarufu mkubwa nchini Marekani.
                                               www.2tayhabari.blogspot.com

0 comments: