Sunday, September 14, 2014

Uwekezaji ulivyoua Mji wa Mirerani-2



SheikhMohammed anasema serikali ndio inawanyanyasa wananchi wake kwa kupitisha sheria ambazo zinawazuia kunufaika na rasilimali za taifa lao ambazo Mungu amewapa.
“Wachimbaji wadogo wamepewa migodi yenye ukubwa wa mita 50 kwa 50 lakini mchimbaji mmoja mkubwa amepewa eneo kubwa zaidi ya eka tano halafu inapitishwa sheria ya kuchimba kwenda chini jambo ambalo haliwezekani huku ni kuwazuia wachimbaji wadogo kupata madini” alisema.
Alisema kwa sasa shughuli nyingi za msikiti huo zimesimama kwani wananchi wa Mirerani hawana fedha za kutoa sadaka tofauti na miaka ya nyuma ambapo sadaka ziliwezesha ujenzi wa msikiti huo, shule na kuwa na miradi.
Padri Aloyce Kitomali wa Kanisa la Katoliki Mirerani, alisema kanisa hilo lilikuwa na uwezo wa kukusanya sadaka katika ibada moja zaidi ya milioni moja lakini sasa hata Sh500, 000 hazipatikani kwani waumini hawana fedha.
Anasema miradi mingi ya kanisa hilo, sasa imezorota kwani wananchi wengi wanategemea madini ya tanzanite ambayo sasa hayapatikani na inasemekana anayepata ni mwekezaji.
“Wananchi hapa wengi wana hali ngumu ya maisha tofauti ya miaka ya nyuma kwani uchumi wao ulitegemea sana madini ya Tanzanite” alisema.
Osca Gunewe ambaye ni Katibu wa Bodi ya shule ya Kanisa la Pentekoste, anasema uchumi wa mji wa Mirerani unategemea madini ya Tanzanite hivyo kwa hali iliyopo sasa ni muhimu Serikali kuwasaidia wakazi wa mji huo.
Gunewe ambaye aliwahi kuwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mirerani, anasema ingewezekana kuwasaidia watu wa Mirerani hata kwa kutolewa ajira kwa vijana wa Mirerani katika migodi ya mwekezaji.
Anasema lakini kampuni hiyo, haiajiri vijana wa Mirerani na hivyo sasa wapo mitaani tu kwani hata migodi ya wachimbaji wadogo mingi imesimama na ambayo inaendelea na kazi, inachukua vijana wachache sana.
Omar Awadhi alikuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mirerani miaka 10 iliyopita, anasema, maisha ya Mirerani sasa yamebadilika na hata uchangiaji shughuli za maendeleo umepungua sana. Anasema Mirerani licha ya utajiri wote, haina hata huduma ya maji safi, kwani ndoo moja inauzwa kati ya Sh400 na 500.
Awadhi anasema maji hayo yanatolewa Wilaya ya Hai Mkoa wa Kilimanjaro kitu ambacho siyo sahihi kulingana na utajiri wa tanzanite ambayo inapatikana Mirerani pekee duniani.
“Tatizo hapa ni mwekezaji kama madini haya yangechimbwa na wachimbaji wadogo pekee hali isingekuwa hivi, kwani watu wengi wangepata madini japo kidogo kidogo lakini yangeendelea kuujenga Mji wa Mirerani na hata mikoa ya jirani,” anasema.

0 comments: