Saturday, September 13, 2014

Shishi Baby: Muziki kwanza, Filamu baadaye

 
 Tathmini iliyofanywa na gazeti hili ni kwamba tangu mwaka uanze, maonyesho aliyofanya mtoto huyu wa kike mwenye mvuto hayapungui 36 na bado yuko kwenye ziara ya Serengeti Fiesta akichanja Mbuga, jana katokea Musoma na leo anaelekea Shinyanga kupiga onyesho la 38 tangu kuanza kwa mwaka wa 2014.
Kikubwa na kinachoshangaza wengi ni kwamba Zuwena Mohamed, a.k.a Shilole ambaye kwa sasa anajitambulisha kwa jina la Shishi baby ni jeshi la mtu mmoja, hana Meneja, anafanya muziki wake mwenyewe na anajisimamia vizuri na kujimudu.
Hakutaka kabisa tumuulize kuhusiana na siri ya mafanikio lakini katufungukia kwa kutuambia kwamba kujiamini na kuongea vizuri na watu ndiko kunasababisha afike alipo sasa, na kila kukicha anaendelea kupiga hatua.
Elimu yake ni kidato cha nne tu na baada ya hapoalisomea mambo ya hoteli, alipomaliza akafanya kazihiyo kwa miezi nane tu, kisha akaenda kwenye sanaa mpaka leo.
Ukiongelea maisha yake ya uhangaikaji, Shishi aliwahi hadi kuuza genge, aliwahi kufanya kazi ya hoteli lakini mwishowe alijikuta akiwa mwigizaji na kwa mara ya kwanza alionekana katika filamu iliyoongozwa na Ray Kigosi, iitwayo Fair decision.
Baada ya hapo akaonekana tena kwenye Mafisadi wa Mapenzi, Bed rest, Morning Alarm, Zawadi ya Birthday na nyingine nyingi.
Baada ya kufanya vizuri kwenye filamu kwa sasa yuko kwenye muziki ambao amekiri unamlipa vizuri na kutoka kote huko kwenye kuuza genge na kufanya kazi za hoteli, sasa ni msanii anayemiliki gari zuri aina ya Harrier lexus pamoja na mgahawa.
Nyimbo zinazompa ulaji kwa sasa ni pamoja na Dume dada, Chuna buzi, lawama, paka la bar, Nakomaa na Jiji, namchukua na Dudu.
Ngoma zote hizi zipo kwenye video na moja tu ndiyo ambayo iko mbioni kutoka, ambayo aliirekodi huko Nairobi Kenya na kampuni ya Diesent Video.
Kila anapokwenda kazini kichwani kwake anawaza sana maisha ya mabinti zake wawili Rahma na Joyce, wanasoma The Click International School, na wengine wa kaka yake Zainab na Hussein ambao pia anawalea na kuwasomesha shule za bweni.
Akiongelea mipango yake ya mbele Shishi ameiambia Starehe kwamba kwanza anamshukuru sana Mungu kwa kukubalika nyumbani na mpango wake mkubwa sasa ni kulichukua soko la kimataifa.
“Siwezi kukwambia nafanya nini kwa sasa lakini kiukweli ni kwamba niko mbioni kurekodi ngoma yenye mtazamo wa kimataifa na kuitupa kwenye media za nje kisha nis’kilizie”, alifafanua Shishi.
                                                www.2dayhabari.com

0 comments: